
SIFA zote njema anastahiki Mwenyezi Mungu Subhānahu Wata‘āla, swala na salamu zimwendee Mtume wetu Muhammad Swallallahu Alayhi Wasallam, maswahaba wake na watangu wema hadi siku ya Kiyama.
Tunapoelekea katika mwezi mtukufu wa Ramadhan, ni wajibu wetu kuukaribisha kwa shauku, furaha, na maandalizi ya kiroho na kimwili. Ramadhan ni mwezi wa rehema, maghfira na ukombozi kutokana na moto wa Jahannam.
Ni fursa adhimu kwa waumini kujitakasa, kujirekebisha na kujikaribisha zaidi kwa Mwenyezi Mungu.
Katika mwezi huu, amri ya kufunga imewekwa juu ya waumini kama alivyosema Mwenyezi Mungu katika Qur’ani Tukufu: “Enyi mlioamini! Mmeandikiwa Saumu kama ilivyoandikwa kwa waliokuwa kabla yenu ili mpate kumcha Mungu.” (Surah Al-Baqarah: 183).
Hii inaonyesha kuwa saumu si tu ibada ya kujizuia na chakula na vinywaji bali ni safari ya kujifunza uchaji Mungu, subira, na kujidhibiti nafsi.
Tunapokaribia Ramadhan, ni vyema tuanze kujiandaa kwa kufanya toba ya dhati kwa Allah, kuondoa kinyongo, chuki, na husuda mioyoni mwetu.
Tuwaombe msamaha wale tuliowakosea na tujiepushe na mambo yote yanayoweza kupunguza thawabu zetu katika mwezi huu mtukufu.
Pia, tujiimarishe katika ibada kama kusoma Qur’ani, kuswali sunna, na kutoa sadaka.
Mtume Swallallahu Alayhi Wasallam alikuwa mkarimu sana katika Ramadhan, kama alivyosimulia Ibn Abbas: “Mtume alikuwa mkarimu sana, na alikuwa mkarimu zaidi katika mwezi wa Ramadhan…” (Bukhari na Muslim).
Ramadhan ni wakati wa kuimarisha uhusiano wetu na Qur’ani kwa sababu ndio mwezi ulioteremsha Kitabu hiki kitukufu.
Mwenyezi Mungu anasema: “Mwezi wa Ramadhan ambao imeteremshwa humo Qur’ani…” (Surah Al-Baqarah: 185).
Hivyo, tujitahidi kuisoma, kuizingatia na kuifuata kwa vitendo.
Kwa kumalizia, tuombe Mwenyezi Mungu atufikishe Ramadhan tukiwa na afya njema, atujaalie tufunge kwa ikhlasi, na atupe fursa ya kujipatia msamaha wake na pepo yake.
Leave a Reply